Swahili New Testament Bible

Matthew 26

Matthew

Return to Index

Chapter 27

1


 

  Kulipopambazuka, makuhani wakuu wote na wazee wa watu walifanya mashauri juu ya Yesu wapate kumwua.  

 

 

--

2


 

  Wakamfunga pingu, wakamchukua, wakamkabidhi kwa Pilato, mkuu wa mkoa.  

 

 

--

3


 

  Hapo, Yuda ambaye ndiye aliyemsaliti, alipoona kwamba wamekwisha mhukumu Yesu, akajuta, akawarudishia makuhani wakuu zile sarafu thelathini za fedha.  

 

 

--

4


 

  Akawaambia, "Nimekosa kwa kumtoa mtu asiye na hatia auawe." Lakini wao wakasema, "Yatuhusu nini sisi? Hilo ni shauri lako."  

 

 

--

5


 

  Naye akazitupa zile fedha Hekaluni, akatoka nje, akaenda akajinyonga.  

 

 

--

6


 

  Makuhani wakuu wakazichukua zile fedha, wakasema, "Haifai kuziweka katika hazina ya Hekalu kwa maana ni fedha za damu."  

 

 

--

7


 

  Basi, wakashauriana, wakazitumia kununua shamba la mfinyanzi liwe mahali pa kuzika wageni.  

 

 

--

8


 

  Ndiyo maana mpaka leo shamba hilo linaitwa Shamba la Damu.  

 

 

--

9


 

  Hivyo maneno ya nabii Yeremia yakatimia: "Walizichukua sarafu thelathini za fedha, thamani ya yule ambaye watu wa Israeli walipanga bei,  

 

 

--

10


 

  wakanunua nazo shamba la mfinyanzi, kama Bwana alivyoniagiza."  

 

 

--

11


 

  Yesu alisimamishwa mbele ya mkuu wa mkoa. Basi, mkuu wa mkoa akamwuliza, "Je, wewe ndiwe Mfalme wa Wayahudi?" Yesu akamwambia, "Wewe umesema."  

 

 

--

12


 

  Lakini makuhani wakuu na wazee walipokuwa wanamshtaki, hakujibu neno.  

 

 

--

13


 

  Hivyo Pilato akamwuliza, "Je, husikii mashtaka hayo yote wanayotoa juu yako?"  

 

 

--

14


 

  Lakini Yesu hakumjibu hata neno moja; hata huyo mkuu wa mkoa akashangaa sana.  

 

 

--

15


 

  Ilikuwa kawaida wakati wa Sikukuu ya Pasaka mkuu wa mkoa kuwafungulia Wayahudi mfungwa mmoja waliyemtaka.  

 

 

--

16


 

  Wakati huo kulikuwa na mfungwa mmoja, jina lake Baraba.  

 

 

--

17


 

  Hivyo, watu walipokusanyika pamoja, Pilato akawauliza, "Mwataka nimfungue yupi kati ya wawili hawa, Baraba*fq* ama Yesu aitwae Kristo?"  

 

 

--

18


 

  Alisema hivyo maana alijua wazi kwamba walimleta kwake kwa sababu ya wivu.  

 

 

--

19


 

  Pilato alipokuwa amekaa katika kiti cha hukumu, mke wake akampelekea ujumbe: "Usijitie katika shauri la mtu huyu mwema, maana leo nimeteseka sana katika ndoto kwa sababu yake."  

 

 

--

20


 

  Lakini makuhani wakuu na wazee wakawashawishi watu waombe Baraba afunguliwe na Yesu auawe.  

 

 

--

21


 

  Mkuu wa mkoa akawauliza, "Ni yupi kati ya hawa wawili mnayetaka nimfungue?" Wakamjibu, "Baraba!"  

 

 

--

22


 

  Pilato akawauliza, "Sasa, nifanye nini na Yesu aitwaye Kristo?" Wote wakasema, "Asulubiwe!"  

 

 

--

23


 

  Pilato akauliza, "Kwa nini? Amefanya kosa gani?" Wao wakazidi kupaaza sauti: "Asulubiwe!"  

 

 

--

24


 

  Basi, Pilato alipotambua kwamba hafanikiwi chochote na kwamba maasi yalikuwa yanaanza, alichukua maji, akanawa mikono mbele ya ule umati wa watu, akasema, "Mimi sina lawama juu ya kifo cha mtu huyu; shauri lenu wenyewe."  

 

 

--

25


 

  Watu wote wakasema, "Damu yake na iwe juu yetu na juu ya watoto wetu!"  

 

 

--

26


 

  Hapo Pilato akawafungulia Baraba kutoka gerezani, lakini akamtoa Yesu asulubiwe.  

 

 

--

27


 

  Kisha askari wa mkuu wa mkoa wakamwingiza Yesu ndani ya ikulu, wakamkusanyikia kikosi kizima.  

 

 

--

28


 

  Wakamvua nguo zake, wakamvika joho la rangi nyekundu.  

 

 

--

29


 

  Kisha wakasokota taji ya miiba, wakamvika kichwani, wakamwekea pia mwanzi katika mkono wake wa kulia. Wakapiga magoti mbele yake, wakamdhihaki wakisema, "Shikamoo mfalme wa Wayahudi!"  

 

 

--

30


 

  Wakamtemea mate, wakauchukua ule mwanzi, wakampiga nao kichwani.  

 

 

--

31


 

  Baada ya kumdhihaki, wakamvua lile joho, wakamvika nguo zake, kisha wakampeleka kumsulubisha.  

 

 

--

32


 

  Walipokuwa wakienda, wakamkuta mtu mmoja jina lake Simoni, mwenyeji wa Kurene, wakamlazimisha kuuchukua msalaba wake Yesu.  

 

 

--

33


 

  Walipofika mahali paitwapo Golgotha, maana yake, "Mahali pa Fuvu la kichwa,"  

 

 

--

34


 

  wakampa mchanganyiko wa divai na nyongo. Lakini Yesu alipoonja akakataa kunywa.  

 

 

--

35


 

  Walimsulubisha, kisha wakagawana mavazi yake kwa kuyapigia kura.  

 

 

--

36


 

  Wakaketi, wakawa wanamchunga.  

 

 

--

37


 

  Juu ya kichwa chake wakaweka shtaka dhidi yake lilioandikwa, "Huyu ni Yesu, Mfalme wa Wayahudi."  

 

 

--

38


 

  Wanyang`anyi wawili walisulubishwa pia pamoja naye, mmoja upande wa kushoto na mwingine upande wa kulia.  

 

 

--

39


 

  Watu waliokuwa wanapita mahali hapo walimtukana wakitikisa vichwa vyao na kusema,  

 

 

--

40


 

  "Wewe! Si ulijidai kulivunja Hekalu na kulijenga kwa siku tatu? Sasa jiokoe mwenyewe. Kama wewe ni Mwana wa Mungu, basi shuka msalabani!"  

 

 

--

41


 

  Hali kadhalika na makuhani wakuu pamoja na walimu wa Sheria na wazee walimdhihaki wakisema,  

 

 

--

42


 

  "Aliwaokoa wengine, lakini kujiokoa mwenyewe hawezi! Eti yeye ni mfalme wa Wayahudi! Basi, sasa na ashuke msalabani, nasi tutamwamini.  

 

 

--

43


 

  Alimtumainia Mungu na kusema eti yeye ni Mwana wa Mungu; basi, Mungu na amwokoe kama anamtaka."  

 

 

--

44


 

  Hali kadhalika na wale waliosulubiwa pamoja naye wakamtukana.  

 

 

--

45


 

  Tangu saa sita mchana mpaka saa tisa, nchi yote ikawa katika giza.  

 

 

--

46


 

  Mnamo saa tisa Yesu akalia kwa sauti kubwa, "Eli, Eli, lema sabakthani?" Maana yake, "Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?"  

 

 

--

47


 

  Lakini wale waliosimama pale waliposikia hivyo wakasema, "Anamwita Eliya."  

 

 

--

48


 

  Mmoja wao akakimbia, akachukua sifongo, akaichovya katika siki, akaiweka juu ya mwanzi, akampa anywe.  

 

 

--

49


 

  Wengine wakasema, "Acha tuone kama Eliya anakuja kumwokoa."  

 

 

--

50


 

  Basi, Yesu akalia tena kwa sauti kubwa, akakata roho.  

 

 

--

51


 

  Hapo pazia la Hekalu likapasuka vipande viwili, toka juu mpaka chini; nchi ikatetemeka; miamba ikapasuka;  

 

 

--

52


 

  makaburi yakafunguka na watu wengi wa Mungu waliokufa wakafufuliwa;  

 

 

--

53


 

  nao, baada ya kufufuka kwake, wakatoka makaburini, wakaingia katika Mji Mtakatifu, wakaonekana na watu wengi.  

 

 

--

54


 

  Basi, jemadari na wale waliokuwa wakimlinda Yesu walipoona tetemeko la ardhi na yale mambo yaliyotukia, wakaogopa sana, wakasema, "Hakika mtu huyu alikuwa Mwana wa Mungu."  

 

 

--

55


 

  Mahali hapo walikuwapo wanawake wengi wakitazama kwa mbali. Hao ndio wale waliomfuata Yesu kutoka Galilaya wakimtumikia.  

 

 

--

56


 

  Miongoni mwao walikuwa Maria Magdalene, Maria mama yao Yakobo na Yosefu, pamoja na mama yao wana wa Zebedayo.  

 

 

--

57


 

  Ilipokuwa jioni, akaja mtu mmoja tajiri mwenyeji wa Armathaya, jina lake Yosefu. Yeye pia alikuwa mwanafunzi wa Yesu.  

 

 

--

58


 

  Akamwendea Pilato, akaomba apewe mwili wa Yesu. Basi, Pilato akaamuru apewe.  

 

 

--

59


 

  Yosefu akauchukua ule mwili akauzungushia sanda safi ya kitani,  

 

 

--

60


 

  akauweka ndani ya kaburi lake jipya alilokuwa amelichonga katika mwamba. Kisha akavingirisha jiwe kubwa mbele ya mlango wa kaburi, akaenda zake.  

 

 

--

61


 

  Maria Magdalene na yule Maria mwingine walikuwa wameketi kulielekea kaburi.  

 

 

--

62


 

  Kesho yake, yaani siku iliyofuata ile ya Maandalio, makuhani wakuu na Mafarisayo walimwendea Pilato,  

 

 

--

63


 

  Wakasema, "Mheshimiwa, tunakumbuka kwamba yule mdanganyifu alisema kabla ya kufa ati, `Baada ya siku tatu nitafufuka.`  

 

 

--

64


 

  Kwa hiyo amuru kaburi lilindwe mpaka siku ya tatu ili wanafunzi wake wasije wakamwiba na kuwaambia watu kwamba amefufuka. Uongo huu wa mwisho utakuwa mbaya kuliko ule wa awali."  

 

 

--

65


 

  Pilato akawaambia, "Haya, mnao walinzi; nendeni mkalinde kadiri mjuavyo."  

 

 

--

66


 

  Basi, wakaenda, wakalilinda kaburi, wakatia mhuri juu ya lile jiwe na kuacha hapo askari walinzi.  

 

 

--

Matthew 28

 

 

 

 

HTMLBible Software - Public Domain Software by johnhurt.com

 


Other Items are Available At These Sites: